NBC Premier League

JKT TANZANIA YAITANDIKA TABORA UNITED LIGI KUU

Published on

JKT Tanzania wakiwa nyumbani kwenye dimba la Azam Complex, Chamazi wamefanikiwa kupata ushindi wa 1-0, goli likifungwa na Maka Edward dakika ya 16 na kuisogeza JKT Tanzania mpaka nafasi ya 5 kutoka nafasi ya 9.

Mchezo ukiwa umetawaliwa na ufundi mwingi hasa kwenye eneo la kiungo, ilikuwa ni burudani kutizama vita ya Najim wawili(Magulu na Mussa ) na tangu dakika za mwanzo za mchezo ni wenyeji ndio walioonyesha kiu hasa ya kupata matokeo na haikuwachukua muda, dk, ya 16 tu ya mchezo walipata bao kupitia kwa Maka Edward aliyefunga bao zuri la kichwa kutokana na krosi maridadi kutoka kwa David Brayson na mpira kummshinda golikipa John Nobel.

Tabora United  walikuwa kama hawapo mchezoni, mfumo wao wa Leo na uchaguzi wa kikosi hasa baadhi ya maneo kuweka watu wasio sahihi kwenye baadhi ya maeneo  iliwagahrimu pakubwa na kufanya makosa yasiyo ya lazima. JKT wangeweza kufunga magoli mengi kipindi hiki cha kwanza kama wangekuwa makini kutumia nafasi zao.

Aaron Lulambo amezoeleka kuonekana akicheza nafasi ya beki wa kulia lakini leo alikuwa akicheza beki wa kati sambamba na Heritier, alikuwa akifanya makosa sana ya kiulinzi. Hata goli walilofunga lilisababishwa na yeye kuwa nje ya nafasi.

Mapumziko,  JKT walienda wakiwa kifua mbele kwa uongozi wa 1-0.

Kipindi cha pili mwalimu Goran alifanya mabadiliko kadhaa ili kuirudisha timu kwenye ukawaida wake, akiwaingiza, Jerome Lambele, Athumani Abbas, Yohana Mkomola na Komanji. Dakika ya 55 JKT pia walifanya mabadiliko kwa kummtoa Hassan Dilunga na Kumuingiza Said Ndemla.

Mchezo ulionekana kutulia ndani ya dakika hizi huku timu zote zikishambuliana kwa wakati. Dakika ya 58 ya mchezo, Sixtus Sabilo alimalizia krosi ya chini chini kutoka kwa Martin Kigi na  kuiandikia timu yake ya JKT bao la pili lakini muamuzi msaidizi alishaonyesha ishara ya kuwa ameotea.

Najim Mussa aliendelea kutamba kwenye eneo la kiungo na kujaribu kuuiendesha timu hasa kwenye ushambulizi. Alipiga pasi nzuri kwa Pauline Kasindi lakini shuti lake lilibabatiza mabeki wa JKT na mpira kuwa kona. Lakini kona haikuwa na faida kwao.

Dakika ya 69, JKT Tanzania walifanya mabadiliko mengine ya kiufundi kwa kumuingiza mshambuliaji asilia Danny Lyanga na kummtoa kiungo mshambuliaji Najim Magulu. Hii limaanisha mfumo kuwa 4-2-3-1, ambapo Sixtus Sabilio, Said Ndemla  na Marti Kiggi wakicheza nyuma ya Danny Lyanga. Maka Edward na Hassan Maulid wakicheza kama viungo wawili wa ulinzi.

Dakika  ya 82, Sixtus Sabilo alipiga pasi kwa Danny Lyanga ambaye naye alifanya mkimbio mzuri na kuingia na mpira ndani ya eneo la penati la Tabora United, akatoa pasi nzuri kwa Said Ndemla ndani ya Sita, lakini akapaisha. Nafasi adhimu wakakosa JKT.

Kilichokuwa kikiwapa faida JKT kipindi chote cha mchezo ni namna walivyokuwa wakifanya majukumu kwa pamoja. Kwenye kukaba na kushambulia. Kuliwanyima kabisa nafasi Tabora United kupanga mashambulizi. Ungeweza kukuta Edson Katanga na George Wawa wapo kwenye kusaidia Mashambulizi na wakati mwingine utammkuta Sabilo au Maka Edward wakisaidia ukabaji. Presha ilianzia juu mpaka kwenye safu ya Ulinzi. Lakini umakini tu wa kumalizia nafasi nyingi walizozitengeneza ndicho kilichokosekana.

Kadi ya kwanza ya mchezo ilikwenda kwa Jerome Lambele baada ya kummchezea vibaya Mohamed Bakari na kuonyeshwa kadi ya Njano ikiwa dakika ya 90 ya mchezo.

Dakika zote 90 zinamalizika kwa JKT Tanzania kuibuka na ushindi wa bao 1-0.

Popular Posts

Exit mobile version