Hii ni orodha ya wachezaji watano (5) wa Young Africans ambao waliwahi kusajiliwa na klabu hiyo wakiwekewa matarajio ya kufanya vizuri lakini hawakufikia kiwango kile ambacho mashabiki walikuwa wanahitaji wafike na pengine wamesahaulika kabisa.
SAID BAHANUZI
Nyota huyu alisajiliwa na klabu ya Yanga akitokea klabu ya Mtibwa Sugar. Wakati akiwa Mtibwa alikuwa ni miongoni mwa nyota wa kutegemewa kwenye eneo la ushambuliaji lakini baada ya kutua mitaa ya Twiga na Jangwani mambo yakawa magumu kwake.
Nyota yake iling’ara zaidi katika mashindano ya Kagame yaliyokuwa yanafanyika Jijini Dar Es Salaam baada ya kumaliza kinara wa upachikaji magoli akiwa na kikosi cha Yanga na baada ya hapo mambo yakamwendea kombo.
Mashabiki wengi wa Yanga pengine watamkumbuka kwa tukio la kukosa mkwaju wa penati dhidi ya Al Ahly pale nchini Misri wakati Yanga ikitafuta nafasi ya kufuzu hatua ya makundi ya Ligi ya mabingwa Barani Afrika.
2. GEILSON SANTOS JAJA
Nyota huyu raia wa Brazil alijiunga na kikosi cha Yanga akitokea nchini kwao Brazil baada ya kusajiliwa na aliyekuwa kocha wa Yanga Marcio Maximo. Mshambuliaji huyo aliimbwa sana na mashabiki wa Yanga wakati akisajiliwa na waliweka matumaini makubwa ya kufanya vizuri lakini mambo yakawa magumu kwa Mbrazili huyu.
Tukio lake la kubwa ambalo pengine mashabiki wa Yanga wanalikumbuka ni pale alipofunga goli kwa mtindo wa ‘Chop’ kwenye mchezo wa ufunguzi wa Ligi kuu soka Tanzania Bara [Ngao ya Jamii] dhidi ya klabu ya Azam fc, mchezo ambao Yanga waliibuka na ushindi na kuwa mabingwa.
3. KPAH SHERMAN
Huyu ni mshambuliaji raia wa Liberia alijiunga na Yanga msimu wa 2014/15 akitokea Cetinkaya TSK ya Cyprus akiwa na matarajio makubwa kwa mashabiki wa Yanga lakini mambo hayakuwa kama ambavyo mashabiki walitarajia.
Sherman alicheza mechi 16 na kufunga magoli 6 pekee na huo ukawa msimu wake wa kwanza na wa mwisho kuitumikia klabu ya Yanga akiwa na miaka 23. Hata hivyo nyota huyo ni Lulu nchini kwao Liberia akiwa na miaka 31 akichezea timu ya Sri Pahang ya Malaysia na anatumika kwenye kikosi cha timu ya Taifa ya Liberia kama nahodha.
4. YOUTHE ROSTAND
Nyota huyu raia wa Cameroon alisajiliwa kutoka klabu ya African Lyon ya Jijini Dar Es Salaam, msimu wa mwaka 2016/17 akisaini mkataba wa miaka miwili chini ya kocha mzambia George Lwandamina ‘Chicken Man’.
Wakati anasajiliwa wengi waliamini kuwa golikipa huyu ataisaidia klabu hiyo hasa katika michuano ya kimataifa lakini mambo hayakuwa hivyo na kwa kiasi kikubwa alichangia timu kutokufanya vizuri, Kocha wa zamani wa Yanga Mwinyi Zahera kipindi akiwa kocha wa Yanga aliwahi kusema;
Anaonekana kuwa kipa mzuri, lakini kwangu mimi ninavyo muona na umri wake aende kusimamia mashamba kwao.
Alisema Mwinyi Zahera baada ya kujiunga na kikosi cha Yanga akichukua nafasi ya George Lwandamina.
5. YIKPE GISLAIN GNAMIEN
Mshambuliaji huyu raia wa Ivory Coast alisajiliwa na kikosi cha Yanga kwa mbwembwe zote akitokea klabu ya Gor Mahia ya nchini Kenya msimu wa 2019/20 akitumika msimu mmoja pekee. Alisajiliwa na Yanga akiwa na miaka 23.
Mashabiki wa Yanga kabla ya kumuona uwanjani walikuwa wakimuimba kuwa huenda ndiye Didier Drogba mpya lakini mambo yakaenda kombo kwa nyota huyu na msimu huo hakufikisha zaidi ya magoli matano (5).